Description
Swala ni nguzo muhimu sana ya dini; na inasemekana kwamba Siku ya Hesabu kitu cha kwanza kuangaliwa ni swala. Kama swala itatakabaliwa na Mwenyezi Mungu, basi huchukuliwa kwamba matendo yote hutakabaliwa pia. Matokeo yake, mtu huyo hupitishwa moja kwa moja kwenye Sirati na kuingizwa Peponi. Mtume (s.a.w.w.) amesema: “Swala ni nguzo ya dini, mwenye kusimamisha swala amesimamisha dini, na mwenye kuicha swala hakika ameiangusha dini.” Mtume (s.a.w.w.) akaendelea kusema: “Tofauti baina yetu na ukafiri ni kuacha (taariku) swala.” Yaani kinachotutofautisha sisi Waislamu na ukafiri ni kuacha swala. Swala ndiyo inayotutofautisha na ukafiri kwa sababu kafiri yeye huwa haswali. Hadithi nyingine kutoka kwa Mtume (s.a.w.w.) inasema kwamba: “Kila kitu kina uso, na uso wa dini (ya Uislamu) ni swala.” Kitu cha kwanza kuonekana katika kila kitu ni uso wake, kama uso ni safi huchukuliwa kwamba kitu chote ni safi, kama uso ni mchafu huchukuliwa kwamba kitu chote hicho ni kichafu. Kwa hivyo, hadithi inatuhimiza kuswali ili kuuweka uso wa dini katika hali ya usafi na dini yetu kwa ujumla iwe safi.